Taarifa kwa Vyombo vya Habari
Written by Stonetown (Kiongozi) // 26/01/2012 // Habari // 3 Comments
Mnamo Januari 26 Mwaka 2001, Chama cha Wananchi, CUF, kiliandaa maandamano halali nchini, kupinga matokeo batili yaliyotangazwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, ZEC.
Serikali kupitia vyombo vya dola, waliamua kutumia nguvu kupita kiasi, kukabiliana na maandamano hayo ambapo pia baadhi ya watendaji wake waliitumia fursa hiyo kutekeleza mauaji na hujuma zilizopelekea maafa makubwa, dhulma, udhalilishaji wa watu, na uharibifu mkubwa wa mali.
Chama cha Wananchi, CUF, kimelazimika kuukumbusha Umma wa Wazanzibari, Watanzania, na Ulimwengu kwa ujumla juu ya matukio ya Januari 26 na 27, mwaka 2001, katika Visiwa vya Unguja na Pemba.
Chama cha CUF kinaamini kwamba maisha, roho, na mali zilizopotea pamoja na athari zake, thamani na gharama yake ni kubwa, na pia si jambo rahisi kusahau maishani na pia si busara kuacha kuzikumbuka.
Lengo ni kuweka mazingatio kwa Serikali, Dola, Mamlaka zinazotawala, Jamii, na Umma kwa ujumla, pamoja na vizazi vijavyo, juu ya umuhimu wa HAKI, DEMOKRASIA, UTAWALA BORA, AMANI, UTULIVU NA THAMANI YA MAISHA YA WATU, ndani na nje ya Taifa hili.
Kwa kushirikiana na Wananchi, Wapenzi, Wanachama, Wafuasi, Raia wema, Ndugu, Jamaa na Marafiki wa WOTE WALIOATHIRIWA AU KUPOTEZA MAISHA, Chama cha CUF kinayakumbuka Mauaji ya Tarehe 26 na 27 Januari 2001, na kinaahidi kuendelea, katika maisha yote, kuheshimu damu iliyomwagika, na pia mchango wao katika kuipigania HAKI, AMANI, NA HESHIMA YA NCHI YAO.
Chama cha CUF KINAMUOMBA MWENYEZI MUNGU (SW) AWAPE MAREHEMU MAKAAZI MEMA PEPONI NA PIA AWAZIDISHIE SUBRA WOTE WALIOGUSWA NA ATHARI ZA MAUAJI HAYO – AMIN.
Pamoja na kumbukumbu hiyo, Chama cha Wananchi-CUF, kimeamua kusisitiza mambo yafuatayo, kama sehemu ya mazingatio ya yale yaliyotokea ambayo sasa tunayakumbuka:
- Utendaji na usimamizi wa HAKI kupitia Misingi ya DEMOKRASIA ili kuhakikisha Nchi inaendelea kubaki katika hali ya AMANI, UTULIVU NA MSHIKAMANO. Hili litawezekana pale ambapo Serikali itaendelea kuwapatia HAKI wananchi zikiwamo za VITAMBULISHO VYA UKAAZI VYA MZANZIBARI, kisheria bila ubaguzi. Hii ni kutokana na kwamba Chama cha CUF kimebaini kwepo ubabaishaji katika Mamlaka inayohusika na Vitambulisho hivyo, ambapo katika hali ya kutatanisha Wazanzibari wanaendelea kunyimwa haki yao hiyo huku wasiokuwa Wazanzibari wakiendelea kupewa Vitambulisho hivyo kwa wepesi.
- Chama cha CUF kinamuomba Raisi wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pamoja na Serikali yake ya Umoja wa Kitaifa, kukemea mara moja UBABAISHAJI HUO, NA PIA KILA AINA YA HILA ZA KUIDHOOFISHA ZANZIBAR NA WANANCHI WAKE.
- Chama cha Wanachi, CUF kinaamini Ofisi ya Mkurugenzi wa Vitambulisho vya Ukaazi vya Mzanzibari, na pia Mamlaka nyingine zenye mwelekeo wa UBABAISHAJI, hawatakuwa na uwezo wa kulipa gharama ya imani na amani waliyonayo Wazanzibari kwa Nchi na Serikali yao.
- Chama cha CUF kinamini Serikali ya Umoja wa Kitaifa itatekeleza ahadi zake zote juu ya yote yaliyohusu au yanayohusu kuzama kwa Meli ya Mv. Spice Islanders, na pia kama ilivyopendekezwa na Kamati ya Kuchunguza Tukio hilo.
- Chama cha CUF kinaiomba Serikali itumie kila uwezo wake kukabiliana na dhulma, ubaguzi, ukandamizaji, ubabaishaji na kila aina ya hujuma za kudhoofisha AMANI, MAENDELEO, MARIDHIANO, UMOJA WA KITAIFA, NA HESHIMA YA ZANZIBAR.
HAKI SAWA KWA WOTE
………………………………………..
Salim Bimani,
MKURUGENZI WA HAKI ZA BINAADAMU NA MAHUSIANO YA UMMA, CUF




3 Comments on "Taarifa kwa Vyombo vya Habari"
mambo yana pita mengi tu ila naona mh Dr shein kimyaaaa!! anatupa waswas sisi wananchi.. ivi yeye haongei? au mpaka kitokee nini yeye ndo ataongea. au Ma Dr hawaongei? hahahahah kaaazi kweli kweli.
dume la nyani alitudhalilisha sana wa ZNZ lakini na sisi sijuwa tunalaaana ya mapinduzi haram ingawa walio fanya wana yaita halali hatufikiri au hatuumii kwa sababu walio fanyiwa wana toka upande mmoja hatujuti alimradi vurugumechi
@kijini.
wewe umeandika dume la nyani commet yako imeachwa .
mimi niliandika NDULI huyo ,basi comment imefutwa jee tutafika au ndio katiba mpya waliopewa zawa?
Naandika tena Tony blair Aliwekwa kiti moto kuhusu Iraq .jee kwanini SUK ISIMUWEKE KITI MOTO HUYU NDULI ?